Jumatatu , 27th Mar , 2023

Happiness William (18) mkazi wa Kijiji cha Nyehunge wilayani Sengerema mkoani Mwanza anashikiliwa na Jeshi la polisi mkoani humo kwa tuhuma za kuiba mtoto mchanga mwenye umri wa miezi sita ili akamuonyeshe mume wake kuwa amejifungua

Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza Wilbroad Mutafungwa amesema tukio hilo limetokea jana tarehe 26 majira ya saa mbili asubuhi katika mtaa wa Migombani kata ya Nyampulukano tarafa ya Sengerema wilayani Sengerema ambapo mtoto huyo aitwaye Anitha Richard mwenye umri wa miezi sita alikuwa anacheza na dada yake aitwaye Martha Richard mwenye umri wa miaka 9 ambae alitumwa kufuata ndoo na aliporudi hamkuta mdogo wake huyo

Baada ya kufika majira ya saa saba mchana mama wa watoto hao aitwaye Agness Robert aliwatafuta Watoto wake ndipo alipogundua kuwa mwanae Anitha hayupo na kuanza kumtafuta bila mafanikio na Kwenda kuripoti katika kituo cha polisi, ndipo msako wa kumtafuta mtoto huyo ukafanyika na kumkuta akiwa amebebwa na Happiness Willliam katika Kijiji cha Nyehunge na kukiri kuhusika na wizi wa mtoto huyo kwa madai kuwa alitaka Kwenda kumuonyesha mume wake kuwa amejifungua na kwamba huyo ndiyo mtoto wake

Aidha kamanda Mutafungwa amesema watu wawili wameliwa na mamba kwa nyakati tofauti ambapo katika mwalo wa mwalo wa Kazunzu kijiji na Kata ya Kazunzu, katika fukwe za ziwa Victoria uliokotwa mwili wa Salome Dotto mwenye umri wa miaka 30 anayedaiwa kufariki kwa kuliwa na mamba ambapo mwili huo umeshafanyiwa uchunguzi na kukabidhiwa kwa ndugu zake

Na katika Kijiji cha Izindabo kata na tarafa ya Buchosha wilayani Sengerema mtu aliyejulikana na Primitiva Evarist mwenye umri wa miaka 56 mkazi wa Izindabo naye alifariki dunia kwa kuliwa na mamba wakati akinawa miguu katika fukwe za ziwa Victoria na kwamba mwili wake umeshafanyiwa uchunguzi na kukabidhiwa kwa ndugu zake.