Jumapili , 28th Sep , 2014

Mwanasiasa Mkongwe nchini Tanzania Kingunge Ngombale Mwiru amesema Katiba ya sasa imezingatia masuala ya Msingi na kuwa bora zaidi na kuongeza kuwa vipengele viliyoondolewa ni kwa maslahi ya Taifa la Tanzania.

Mwanasiasa mkongwe nchini Tanzania, mzee Kingunge Ngombare Mwiru.

Akichangia rasimu iliyopendekezwa leo bungeni mjini Dodoma Kingue amesema hata kuondolewa kwa mfumo wa Serikali Tatu ni kwa kuwa muundo huo ulikua umelenga kuuvunja muungano jambo ambalo halitakua na maslahi ya Taifa.

Kingunge amesema Katiba ya sasa ni bora kwa kuwa imezungumzia utatuzi wa matatizo mbalimbali ya Wananchi na Kuongeza kuwa ili kuweza kupata heshima na kuwaenzi waasisi wa Taifa ni Kutengeneza katiba bora itakayoimarisha Muungano.

Aidha katika hatua nyingine, mjumbe wa bunge hilo, Stephen Wassira, yeye ametaka Katiba Mpya inayopendekezwa, iruhusu kila raia anaejua kusoma na kuandika kugombea nafasi mbalimbali za uongozi, kwa kuwa suala la kushika madaraka ni haki ya kila Mtanzania.

Wassira ambaye pia ni mbunge wa Bunda mkoani Mara, ametoa pendekezo hilo mjini Dodoma, wakati wa kuchangia rasimu ya Katiba Inayopendekezwa, na kutahadharisha kuwa elimu isiwe kigezo cha kuwazuia raia haki yao ya msingi ya kushiriki katika kuiongoza nchi yao.

Wasira ameongeza kuwa mazingira ya elimu nchini yameshindwa kuwaandaa Watanzania wote kuwa na elimu ya juu na kwamba kuna idadi kubwa ya Watanzania wana uwezo wa kuongoza licha ya kuwa na kiwango kidogo cha elimu.