Jumanne , 7th Oct , 2014

Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la chama cha Demokrasia na Maendeleo BAWACHA ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Kawe jijini Dar es salaam Mhe. Halima Mdee leo amefikishwa katika mahakama ya hakimu mkazi Kisutu.

Mbunge wa Jimbo la Kawe kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Bi. Halima James Mdee.

Mdee amefikishwa katika mahakama hiyo pamoja na wanachama wengine wanane wa chama hicho na kusomewa mashtaka mawili ya kukusanyika kinyume cha sheria pamoja na kutotii amri halali ya polisi.

Akiwasomea mashataka hayo, Wakili wa serikali Mohamed Salim amesema Mhe. Mdee pamoja washtakiwa wengine wanane walikusanyika Oktoba 4, mwaka huu katika mtaa wa ufipa kinondoni Dar es salaam kwa lengo la kuelekea Ikulu jijini Dar es salam na walikataa amri halali ya polisi ya kutawanyika.

Washtakiwa wote tisa wamekana mashtaka, ambapo upelezi wa kesi hiyo umekamilika na washtakiwa hao watasomewa maelezo ya awali Oktoba 21 mwaka huu katika mahakama hiyo.

Katika hatua nyingine, Serikali imeondoa zuio la mikutano ya vyama vya siasa lililokuwa limewekwa katika mikoa ya Lindi na Mtwara kutokana na vurugu za wananchi waliokuwa wakipinga ujenzi wa mradi wa bomba la gesi kutoka Mtwara kwenda Dar es salaam.

Katika taarifa iliyosambazwa kwa vyombo vya habari leo na Waziri wa Mambo ya Mdani Mathias Chikawe, amesema hatua hiyo imechukuliwa na serikali baada ya kuridhika kuwa hali ya amani na utulivu imerejea katika mikoa hiyo na kuwa mikutano hiyo sasa inaweza kuendelea kufuatia sheria na utaratibu uliowekwa.

Aidha Waziri Chikawe amesema jeshi la Polisi litaendelea kutoa ushirikiano katika uendeshaji wa mikutano ya kisiasa inayoendelea maeneo mbalimbali nchini na kuvitaka vyama vya siasa kutumia fursa hiyo kwa kuendesha mikutano yao kwa amani na utulivu.