Alhamisi , 15th Dec , 2016

Waziri wa Elimu , Sayansi, Teknolojia na Ufundi Profesa Joyce Ndalichako, amewataka Makatibu Tawala na Wakurugenzi kote nchini, kuhakikisha wanawalinda wakuu wa shule wanaoingiliwa mamlaka zao na wanasiasa.

Waziri wa Elimu, Prof Joyce Ndalichako

 

Ndalichako ametoa kauli hiyo leo mjini Dodoma katika mkutano mkuu wa 11 wa wakuu wa shule za sekondari nchini (Tahossa).

Amesema kumekuwapo na tabia ya baadhi ya wanasiasa kuingilia mamlaka za walimu wakuu kwa kuamuru waondolewe kutokana na kutokubaliana nao katika mambo ya kiutawala.

Amesema anawaagiza makatibu tawala na wakurugenzi nchini kote, kuhakikisha wanawasimamia na kuwalinda walimu wakuu wa shule ambao mara kwa wanaingiliwa majukumu yao na kupewa vitisho na baadhi ya wanasiasa.

"Imekuwa tabia kwa baadhi ya wanasiasa kutoa maagizo ambayo si ya kitaaluma kwa wakuu wa shule na kuwaondosha katika mstari wa kufanya taaluma yao kimaadili" Amesema Ndalichako