Jumatatu , 13th Apr , 2015

Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama barabarani limewaonya wamiliki wa mabasi ya abiria kuacha tabia ya kuwaamuru madereva wao kwenda mwendo wa kasi na kwamba halitasita kuchukua hatua dhidi ya wamiliki hao.

Aidha, jeshi hilo pia limesisitiza umuhimu wa madereva wote wa vyombo vya moto nchini kwenda kusoma kwani hatua hiyo itawapa umahiri wa kazi yao na hivyo kupunguza kiwango cha tatizo la ajali za barabarani zinazotokea takribani kila siku hapa nchini.

Mnadhimu Mkuu wa Kikosi cha Usalama barabarani, Johansen Kahatano, amesema hayo leo katika mahojiano na East Africa Radio, ikiwa ni siku chache tangu kufanyike kwa mgomo wa madereva wote wa vyombo ya moto nchini, ambao walikuwa wakipinga mazingira mabovu ya kazi na kukosekana kwa mfumo bora wa ajira ya udereva.