Jumatatu , 21st Dec , 2015

Serikali ya Tanzania imesema kuwa inakusudia kuboresha mifumo yote ya ulinzi na kuimarisha ulinzi nchini ili kukabiliana na uhalifu wa namna mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuongeza nguvu katika uthibiti wa biashara ya dawa za kulevya.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga (katikati) akimsalimia Naibu Mkuu wa Jeshi la Polisi (D/IGP), Abdurahman Kaniki

Hayo yameelezwa leo jijini Dar es Salaam na Waziri wa Mambo ya ndani ya Nchi, Mh. Charles Kitwanga, wakati akiongea na watendaji wa idara mbalimbali wa Jeshi la Polisi nchini katika kueleza mambo mbalimbali yanayohitaji maboresho katika jeshi hilo.

Aidha, Mh. Kitwanga amesema kuwa wataendelea pia kuhakikisha kuwa polisi wanajengewa mazingira bora kazini na nyumba ili kuboresha utendaji wa kazi zao ili waweze kuimarisha usalama nchini.

Kwa upande wake Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Tanzania IGP Ernest Mangu amesema kuwa jeshi hilo pia linawatafuta watu wanaoeneza habari zisizo na ukweli kwenye mitandao ya kijamii juu ya madai ya kuwepo kwa askari waliojiunga na jeshi la polisi kwa kutumia vyeti vya kughushi.