Ijumaa , 5th Sep , 2014

Jumuiya ya Wafanyabiashara nchini Tanzania JWT imeishutumu mamlaka ya mapato nchini TRA kwa kuchochea hatua ya baadhi ya wafanyabiashara nchini kufunga maduka yao kupitia utata unaoendelea kuhusu matumizi ya mashine za risiti za kielektroniki za EFD.

Baadhi ya maduka yakiwa yamefunguliwa kwa kuvizia katika mitaa ya Kariakoo jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa JWT Bw. Johnson Minja, amesema hayo leo wakati akizungumzia mkutano mkubwa wa wafanyabiashara wa nchi nzima utakaofanyika mjini Dodoma kesho, na kufafanua kuwa hatua hiyo inatokana na kitendo cha TRA kufunga maduka ya wafanyabiashara wasio na mashine za EFD wakati ambapo serikali pamoja na wawakilishi wa wafanyabiashara wakiendelea kulijadili suala hilo.

Minja amefafanua kuwa kimsingi wafanyabiashara hawakati kulipa kodi pamoja na matumizi ya mashine za EFD, isipokuwa mzima wa ulipaji kodi nchini, mfumo ambao wamesema umekuwa ukiwanufaisha wachache kuua biashara, badala ya kuongeza mapato kwa serikali.

Kauli ya wafanyabiashara hao imekuja siku moja baada ya mamlaka ya mapato nchini TRA kudai kuwa suala la wafanyabiashara kugomea mashine za EFD pamoja na kufunga maduka yao limekuwa likichochewa na baadhi ya wafanyabiashara wenye maslahi binafsi.