Alhamisi , 20th Aug , 2015

Kizungumkuti kimeendelea kujitokeza katika jimbo la Mtwara mjini ambapo mpaka sasa ni jumla ya wagombea wa vyama vitatu vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA wamechukuwa fomu kwa ajili ya kugombea jimbo hilo.

Mgombea wa jimbo la Mtwara Mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Joel Nanauka.

Wagombea hao ambao wamechukua fomu hizo huku wakisubiri uamuzi wea vikao vya juu ambapo kesho ndiyo mwisho wa kurejesha fomu za kuwania nafasi hiyo ni Joel Nanauka (CHADEMA), Hasnain murji (CCM), Hassan Uledi (NCCR) na Maftaha Nachuma (CUF).

Akizungumza mara baada ya kuchukua fomu Mgombea wa jimbo hilo kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Joel Nanauka, aliwataka wananchi wa Mtwara kuendelea kuwa watulivu na kusubiri maamuzi yatakayotolewa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) juu ya chama gani kinapaswa kusimamisha mgombea katika jimbo hilo.

Wakati hayo yakiendelea mbunge wa Mtwara mjini anayemaliza muda wake, Mhe. Hasnain Murji, amesema hatishwi na mgombea yeyote wa vyama vya upinzani ambao wamechukuwa fomu kwa ajili ya kugombea katika jimbo hilo.

Murji aliyasema hayo jana baada ya kuchukua fomu ya ugombea katika ofisi ya mkurugenzi wa manispaa ya Mtwara Mikindani, Limbakisye Shimwela, na kufanya idadi ya waliochukuwa fomu hadi jana kuwa ni wanne.