Alhamisi , 12th Jun , 2014

Ulinzi mkali uliimarishwa viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha leo asubuhi, huku waandishi wa habari wakipekuliwa mikoba yao kabla ya kuingia ndani ya Chumba cha mahakama ya hakimu mkazi Arusha.

Hali hiyo imetokea wakati watuhumiwa tisa wa mlipuko wa bomu, uliotokea baa ya Arusha Night Park, walipofikishwa mbele ya Hakimu Mfawidhi Mustapher Siyani, kwa mara ya pili, kujibu mashtaka 16 ya kuua na kujaribu kuua.

Askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) wakiwa kwenye gari la polisi waliokuwa kwenye sare, askari kanzu na baadhi yao wakiwa wanaranda randa na mbwa kuzunguka eneo lote la Mahakama ndani na nje ya mahakama hiyo, walionekana kutanda kila kona mahakamani hapo asubuhi hadi kesi ilipotwajwa tena majira ya saa 4 na dakika 40.

Watuhumiwa hao wamepakiwa kwenye basi la Magereza, chini ya ulinzi mkali, huku nyuma likifuatwa na gari lililosheheni askari wa magereza na FFU, yaliingia mahakamani hapo kwa kasi, hali iliyowafanya baadhi ya watu kutoka ndani ya vyumba vya mahakama kuangalia.

Wakati wa kutajwa kesi hiyo Mwendesha Mashataka Wakili wa Serikali Hellen Rwijage, amemwomba Haimu wa Mahakama hiyo Siyani kuairisha kesi hiyo hadi tarehe juni 25 kutokana na upelelezi kutokamilika.

Awali kesi hiyo ilisomwa na wakili wa Serikali Marcelino Mwamunyange ambapo alidai mahakamani hapo kuwa watuhumiwa hao April 13 mwaka huu saa 1:30 usiku kwenye baa ya Night Park, walilipua bomu na kusababisha majeruhi na kusababisha kifo cha Sudi Ramadhani, kushawishi vijana kujiunga katika kikundi cha kigaidi cha al Shabaab.