Alhamisi , 2nd Oct , 2014

Serikali imetakiwa kuifanyia mabadiliko sheria ya kazi ya mwaka 1999 kwani haiendani na mazingira ya sasa ya kiuchumi.

Mkurugenzi Mtendaji wa chama cha waajiri nchini Tanzania - ATE, Dkt Aggrey Mlimuka.

Mkurugenzi Mtendaji wa chama cha waajiri nchini Tanzania ATE Dkt Aggrey Mlimuka, amesema hayo leo wakati wa mkutano wa mwaka wa ATE uliofanyika jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Dkt Mlimuka, moja ya maeneo ambako kutahitajika sana sheria bora ya kazi ni katika sekta mpya za kiuchumi za mafuta na gesi ambako amesema sheria bora ya kazi itawezesha upatikanaji wa ajira zenye staha na maslahi bora kwa waajiriwa.

Wakati huo huo, imeelezwa kuwa Kiwango cha ukuaji uchumi nchini Tanzania kitaongezeka iwapo wananchi watailinda na kuitumia sawasawa miundombinu ya barabara katika usafirishaji wa mazao na bidhaa mbali mbali.

Rais Jakaya Mrisho Kikwete ametoa wito huo leo wakati akizundua barabara kati ya Mwenge na Tegeta, yenye urefu wa kilomita 12.9 ambapo amesema kukamilika kwa barabara hiyo na nyingine nchini ni kichocheo kizuri cha uchumi.

Rais Kikwete amesema serikali inatumia kiasi kikubwa cha pesa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu na kwamba ni jukumu la wananchi kuilinda miundombinu hiyo na kuitumia kwa biashara na kukuza kipato.