Jumanne , 23rd Apr , 2024

Zaidi ya wanafunzi 80,000 wa shule za msingi katika wilaya za Rufiji na Kibiti mkoani Pwani wamekosa masomo kufuatia mafuriko yaliyotokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha.

Ofisa Elimu mkoa wa Pwani, Sara Mlaki, ameyasema hayo kwenye ziara ya kujionea athari za mvua hizo katika shule na makazi katika wilaya za Rufiji na Kibiti ikiwamo kuharibu  miuondombinu ya elimu.

Amesema shule 11  za msingi zenye wanafunzi 7,264 wakiwemo wasichana 3,657 na wavulana 3607 wameathirika na mafuriko wilayani Rufiji.

Aidha nyumba 58 za walimu pia zimeathiriwa na kupoteza samani na mali zilizokuwemo ndani ya nyumba hizo.

Amesema katika  wilaya ya Kibiti wanafunzi 824 katika shule 7 za msingi zimeathirika huku 3 zikifungwa kutokana na adha hiyo huku sekondari ya Mtanga Delta  ikiathirika pia.
Akizungumzia maafa hayo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolph Mkenda, alisema tayari serikali imeweka utaratibu kwa wanafunzi wote waliokumbwa na mafuriko hayo kusoma kwenye shule maalum ambazo zimetengwa.