Jumanne , 27th Oct , 2015

Mwanamuziki mkongwe wa muziki wa kizazi kipya nchini, Joseph Haule ( Profesa Jay ) ameshinda kiti cha ubunge jimbo la Mikumi mkoani Morogoro kwa tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo ( CHADEMA).

msanii wa muziki Joseph Haule aka Profesa Jay akiwa na msanii Joseph Mbilinyi aka Mr. II Sugu

Akitangaza matokeo hayo, msimamizi wa uchaguzi huo ambaye ni mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Kilosa, Bw Idd Mshiru amesema katika uchaguzi huo, Joseph Haule ( Profesa Jay ) ameshinda baada ya kupata jumla ya kura 32,256.

Hapo jana jioni msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Mbeya Mjini alitangaza matokeo ya ubunge ambapo mgombea wa jimbo hilo kupitia Chadema, Joseph Mbilinyi, maarufu kwa jina la Mr. II Sugu aliibuka mshindi baada ya kuwabwaga vibaya wagombea wenzake watano aliokuwa akichuana nao.

Kwa mujibu wa Dk. Lazaro, Sugu ameshinda kwa kupata kura 97,675 akifuatiwa na mpinzani wake wa karibu, Sambwee Shitambala wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) aliyepata kura 46,894 huku nafasi ya mgombea wa chama cha ACT-Wazalendo – Amimu Asheri akitupwa nafasi ya tatu kwa kupata kura 696.