Jumatatu , 5th Jan , 2015

MICHUANO ya Judo Kanda ya Tano iliyokuwa ikitarajiwa kufanyika Januari 20 hadi 25 Tanzania ikiwa nchi wenyeji, sasa itafanyika Februari 10 hadi 15 mwaka huu mjini Moshi kwa kushirikisha nchi zaidi Sita.

Akizungumza na East Africa Radio, Katibu Mkuu wa Chama cha Judo nchini JATA, Innocent Malya amesema, mwisho wa nchi shiriki kuhakiki ushiriki wa michuano hiyo ni leo ambapo mpaka ifikapo Januari 10 nchi zote zinatakiwa kuhakiki majina ya wachezaji, uzito wa wachezaji, idadi ya viongozi na wachezaji watakao shiriki katika michuano hiyo.

Malya amesema, wameshatuma barua kwa nchi zote shiriki ambapo wamekubaliana na ratiba hiyo, hivyo wanawasiliana na viongozi wa vilabu shiriki ili kuweza kukutana na kuweza kupanga ratiba nzima ya michuano hiyo.

Malya amesema Timu ya Tanzania inaendelea na kambi ikiwa ni sehemu ya maandalizi hayo huku akiwaomba watanzania kujitokeza kwa wingi katika michuano hiyo kwa ajili ya kuweza kuishangilia timu ya Tanzania ambao ni mabingwa mara mbili mfululizo katika michuano hiyo.