Ijumaa , 3rd Jun , 2016

Chama cha Mpira wa Magongo [hockey] Mkoa wa Dar es salaam DRHA kinataraji kuendesha kwa mara ya kwanza ligi ndefu ya mchezo huo kwa ngazi ya mkoa ambayo inataraji kuanza kesho ikishirikisha vilabu vya wanawake na wanaume kutoka mkoani humo.

Baadhi ya wachezaji wakichuana katika moja ya mashindano ya vilabu.

Zaidi ya vilabu 28 vya mchezo wa mpira wa magongo kwa wanawake na wanaume mkoa wa Dar es Salaam vinataraji kushiriki michuano ya ligi ya mkoa itakayoanza kesho katika viwanja vya JMK Youth Park vilivyoko kidongo chekundu Mnazi mmoja jijini Dar es Salaam.

Katibu mkuu wa chama cha mpira wa magongo mkoa wa Dares Salaam DRHA Mnonda Magani amesema mashindano hayo pamoja nakutoa vilabu bingwa wa mkoa kwa wanawake na wanaume pia yatatumika kung'amua vipaji vipya kwaajili ya kuteua timu ya mkoa itakayoshiriki michuano mbalimbali ya kitaima na kimataifa.

Aidha Magani ambaye pia ni kocha wa mchezo huo amesema michuano hiyo itachezwa kwa mtindo wa ligi ambayo itaanza rasmi kesho na kumalizika mwezi Septemba mwaka huu.

Kabla ya kuanza kwa michuano hiyo jioni kesho asubuhi kutaendeshwa kliniki maalumu ya mafunzo ya sheria za mchezo huo kwa waamuzi na walimu na viongozi ili kukumbushana, kliniki ambayo itaanza saa nne asubuhi mpaka saa kumi jioni yatakapoanza rasmi mashindano yenyewe.

Timu zote 28 zilizothibitisha ushiriki wa ligi hiyo zimegawanywa katika makundi mawili ya A na B kwa pande zote wanawake na wanaume ambapo kwa upande kwa wanaume wao watakuwa na vilabu 19 huku wanawake wakiwa na vilabu 9 ambavyo vitachuana kwa michezo miwili kila mmoja kwa mtindo wa nyumbani na ugenini.