Jumamosi , 4th Jun , 2016

Hatimaye baada ya miaka 19 Mhispania wa kwanza Garbine Muguruza amefanikiwa kumshinda mchezaji namba moja duniani kwa wanawake mchezo wa tenisi Mmarekani Serena Williams na kushinda taji la michuano ya Wazi ya Ufaransa [French Open 2016].

Garbine Muguruza akishangilia baada ya kumshinda Serena Williams katika fainali ya French Open.

Raia huyo wa Hispania Garbine Muguruza ameshinda mchezaji namba moja kwa ubora duniani kwa upande wa wanawake Serena Williams kwa seti za mfululizo na kutwaa taji lake la kwanza kubwa la michuano ya tenisi Grand Slam la michuano ya Wazi ya Ufransa [French Open].

Mchezaji huyo namba nne kwa ubora alishinda kwa seti mfululizo kwa 7-5 na 6-4 na kulipa kisasi chakupoteza fainali ya michuano ya Wimbledon mwaka jana dhidi ya mpinzani wake huyo Serena Williams.

Mwanadada huyo wa Kihispania mwenye umri wa miaka 22- anakuwa mwanamke wa kwanza Muhispania kutwaa taji kubwa la ubingwa huo huko Roland Garros tangu alipofanya hivyo mwanadada Arantxa Sanchez-Vicario mnamo mwaka 1998.

Serena Williams, mwenye umri wa miaka 34, alikuwa na matumaini ya kushinda taji kubwa la 22 la Grand Slam kwa mchezaji mmoja mmoja yaani singles title na kufikia rekodi ya mwanadada Steffi Graf's.

Akizungumzia ushindi wake mwanadada huyo akiwa na furaha amesema " Najisikia raha sana sana kucheza michuano mikubwa ya Grand Slam tena dhidi ya mmoja wa wachezaji bora kabisa duniani, ni fainali safi na bora," alisema Muguruza na kuongeza "Nina furaha sana. Nilikuwa tayari sana na makini katika kila alama na nilipigana kwa uwezo wangu wote kama nilivyoweza".

"Michezo yote niliyocheza dhidi ya Serena ilinisaidia. Ni michuano yakujivunia kwa Wahispania na napenda kuwashukuru mashabiki wote wa Hispania kwa kuniunga mkono," alimaliza mwanadada huyo.