Jumatano , 23rd Nov , 2022

Dakika 90 za mechi ya Mbeya City imemalizika kwa timu hizo kutoa sare ya bao 1-1 huku mabao ya Mzamiru Yassin (Simba) na Tariq Seif yakitosha kumaliza mtanange huo.

Licha  ya kiungo Mzamiru Yassin kufunga bao la kuongoza mbele ya Mbeya City ngoma ilikuwa nzito kwa timu hiyo kuvuna pointi tatu.

Bao la utangulizi lilifungwa dakika ya 14 na kuwafanya Simba kwenda mapumziko wakiwa wanaongoza kwa bao 1-0.

Ngoma ilipinduka kipindi cha pili ambapo kasi ya Mbeya City ilikuwa kubwa mwanzo mwisho kuikabili Simba.

Umakini hafifu wa safu ya ushambuliaji, kiungo wa Simba uliwafanya watunguliwe bao dakika ya 78 kupitia kwa Tariq Seif.

Sasa Simba ina kibarua kingine kuikabili Polisi Tanzania ukiwa ni mchezo wao wa ligi ugenini chini ya Kocha Mkuu, Juma Mgunda.

Hii inakuwa sare ya pili kwa timu hizo katika michezo 15 waliyocheza huku ikiwa ya pili tena kwa Simba msimu huu baada ya kulazimishana bao 1-1 na Singida Big Stars ikiwa ugenini.