Jumamosi , 17th Oct , 2020

Mabingwa wa ligi kuu ya Tanzania bara, Simba itakosa huduma za mshambuliaji wake, Meddie Kagere ambaye atakaa nje ya uwanja kwa wiki tatu kufuatia kukumbwa na majeruhi.

Mfungaji bora kwa misimu miwili katika VPL meddie Kagere akishangilia baada ya kupachika bao.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Simba, Haji Manara amesema kwamba Kagere alipata majeraha akiwa na timu yake ya taifa ya Rwanda hivyo hatokuwepo kwenye kikosi cha wekundu kinachojiwinda na mchezo ujao wa VPL dhidi ya Tanzania Prisons utakaopigwa Oktoba 22 katika dimba la Nelson Mandela mkoani Rukwa.

''Kwa taarifa kutoka kwa daktari wetu ni kwamba mshambuliaji wetu Meddie Kagere atakaa nje kwa wiki tatu hivyo hatutokua naye kwenye safari ya kuelekea mkoani Rukwa, ni pigo kwetu lakini bado tuna kikosi kipana chenye machaguo mengi hivyo tunahuakika tutashinda dhidi ya Prisons wiki ijayo'' alisema Manara.

Katika hatua nyingine Manara amesema nyota wao Gerson Fraga amerejea mazoezini na anaendelea vyema hivyo upo uwezekano wa kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Mlandege itakayopigwa usiku wa leo katika uwanja wa Azam Complex.

Kukosekana kwa Kagere katika kikosi cha Simba ni pigo kwakuwa ameifungia timu hiyo mabao manne na ndiye kinara wa kupachika mabao kwa misimu miwili iliyopita.