Jumanne , 24th Mar , 2015

Timu ya Taifa ya Tanzania Taifa Stars imewasili leo jijini Mwanza, tayari kwa maandalizi ya mchezo wa kirafiki wa Kimataifa Machi 29 dhidi ya timu ya Taifa ya Malawi The Flames, mechi itakayochezwa kwenye dimba la uwanja wa CCM Kirumba.

Kikosi cha Stars kimeondoka kikiwa na wachezaji 18 ambao wameripoti kambini jana, huku kiungo mshambuliaji Mwinyi Kazimoto anayecheza soka la kulipwa nchini Qatar akitarajiwa kuungana na wenzake leo.

Wachezaji waliopo kambini jijini Mwanza ni Magolikipa Aishi Manula na Mwadini Ali wa Azam FC, walinzi ni Erasto Nyoni, Shomary Kapombe, Aggrey Morris wa Azam FC, Salim Mbonde wa Mtibwa Sugar, Haji Mwinyi wa KMKM, Hassan Isihaka na Abdi Banda (Simba SC)

Wengine ni Amri Kiemba, Frank Domayo, Salum Abubakar (Azam FC), Said Ndemla (Simba SC), Haroun Chanongo (Stand United), John Bocco (Azam FC), Juma Luizio (Zesco United), Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe).

Mchezaji Mcha Khamis wa Azam FC amejiondoa kikosini kutokana na kuwa majeruhi, huku wachezaji wa Young Africans wakitarajiwa kujiunga na kikosi hicho cha timu ya Taifa mara tu baada ya mchezo wao wa Ligi Kuu ya Vodacom dhidi ya JKT Ruvu siku ya Jumatano.

Msafara wa watu 25 wa timu ya Taifa ya Malawi (The Flames) unatarajiwa kuwasili jijini Dar es salaam siku ya Alhamis, kabla ya kuunganisha ndege siku ya Ijumaa kuelekea jijini Mwanza tayari kwa mchezo wa kirafiki wa kimataifa dhidi ya Taifa Stars siku ya jumapili.

Katika msafara huo utakaokuwa na wachezaji 18 na viongozi 7, kocha mkuu wa The Flames Young Chimodzi amewajumuisha wachezaji nane (8) katika kikosi chake wanaocheza soka la kulipwa katika nchi za Afrika Kusini, Congo DR, Msumbuji na Zimbabwe.

Wachezaji wanaocheza soka la kulipwa nchini Afrika Kusini ni Limbikani Mzava (Celtic), Harry Nyirenda (Black Leopards), Esau Kanyenda (Polokwane City), na Atusaye Nyondo (University of Pretoria).

Wengine ni Nahodha Joseph Kamwendo (Tp Mazembe - Congo DR), Frank Banda (HBC Songo - Msumbuji), Chimango Kayira (Costal De Sol - Msumbuji) na Gerald Phiri (Caps United - Zimbambwe).