Ijumaa , 9th Jan , 2015

Mechi za kwanza za raundi ya Kwanza za mashindano ya Taifa ya mpira wa miguu kwa wanawake (Taifa Cup Wanawake) zinatarajiwa kuanza kuchezwa kesho katika mikoa 11 tofauti nchini.

Akizungumza jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa Mashindano wa Shirikisho la Soka nchini TFF, Boniface Wambura amesema katika mashindano hayo Geita itakuwa mwenyeji wa Kagera Uwanja wa Geita, Tabora itacheza na Kigoma kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora, Simiyu na Shinyanga itacheza uwanja wa Simiyu, Arusha na Manyara itacheza uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid, na Kilimanjaro na Tanga zitacheza uwanja wa Ushirika.

Wambura amesema mechi nyingine ni Lindi itaikaribisha Mtwara kwenye uwanja wa Ilulu, Ruvuma na Njombe (Uwanja wa Majimaji), Mbeya na Iringa (Uwanja wa Sokoine), Katavi na Rukwa (Uwanja wa Katavi), Dodoma na Singida (Uwanja wa Jamhuri) na Pwani itakuwa mwenyeji wa Morogoro katika uwanja wa Mabatini.

Wambura amesema, timu hizo zitarudiana Januari 13 mwaka huu, ambapo baada ya matokeo ya nyumbani na ugenini timu iliyoshinda ndiyo itakayoingia hatua inayofuata ambayo pia itashirikisha mikoa ya kisoka ya Ilala, Kinondoni na Temeke.

Wambura amesema, hatua hiyo, mechi zake za kwanza zitachezwa Januari 17 mwaka huu wakati zile za marudiano zitafanyika Januari 21 mwaka huu huku hatua ya robo fainali, nusu fainali na fainali ambayo ndiyo itakayotoa bingwa wa michuano hiyo inayofanyika kwa mara ya kwanza nchini.