Jumanne , 6th Jan , 2015

RAIS wa Shirikisho la Soka nchini TFF, Jamal Malinzi amewataka waamuzi mbalimbali hapa nchini kuepukana na vishawishi kutoka kwa watu mbalimbali wenye uwezo wa kuwashawishi waamuzi wakati wa mechi.

Akizungumza jijini Dar es salaam wakati wa kugawa beji za Shirikisho la Soka Ulimwenguni FIFA kwa waamuzi 18, Malinzi amesema iwapo waamuzi hao wataweza kuepukana na vishawishi hivyo, watakuwa na uwezo mkubwa wa kuweza kuchezesha michuano mikubwa ya ndani na nje ya nchi.

Malinzi amesema hivi sasa Tanzania inaongoza kwa kuwa nchi ya ya Pili Barani Afrika kwa kuwa na idadi kubwa ya waamuzi ambapo kwa mwaka jana kulikuwa na waamuzi 13, huku wanawake wakiwa ni wawili na wanaume 11 tofauti na mwaka huu ambapo idadi imeongezeka na kuwa na waamuzi wa kike wakuwa saba na wanaume 11.

Malinzi amesema waamuzi hao wanatakiwa kuwa na uvumilivu katika kazi yao kwani uchaguzi wa waamuzi hao imeangaliwa uwezo walionao hivyo kutasaidia kuweza kuchezesha mechi kubwa na kuweza kupata heshima.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa TFF, Mwesigwa Celestine amesema, mara nyingi mashabiki hufikiria wachezaji ndio wenye uwezo wa kufikisha mbali soka hapa nchini bila kufikiria kuwa mwamuzi ana uwezo mkubwa katika mechi, hivyo wanatakiwa kupewa heshima kama kiongozi wa mchezo anapokuwa uwanjani.

Kwa upande wake mmoja wa waamuzi waliopata Beji hizo, Israel Nkongo amesema waliopata beji hizo wanatakiwa kuzitumia hususani katika mazoezi kwani kila mwaka wakiwa wanapokea waamuzi wapya na wale wa zamani wanatoka inakuwa vigumu kuzilinda Beji hizo kama ilivyoagizwa.

Kwa upande wake, mmoja wa waliopokea Beji hizo kwa upande wa wanawake, Josephine Mduma amesema TFF inatakiwa kuongeza juhudi katika kutoa mafunzo ya waamuzi kwa wanawake ili kuongeza idadi ya waamuzi kwa upande wa wanawake hapa nchini ambao watakuwa na uwezo wa kuchezesha hata Fainali za Kombe la Dunia.