Jumatano , 7th Jan , 2015

VILABU shiriki vya Ligi Daraja la kwanza vimeliomba Shirikisho la Soka nchini TFF kufanya ukarabati wa viwanja vinavyotumika katika ligi hiyo.

Akizungumza na East Africa Radio, Kocha wa timu ya Villa Squard, Habibu Kondo amesema viwanja mbalimbali vimekuwa havina uzio unaotenganisha kati ya wachezaji na mashabiki suala linaloweza kuleta vurugu wakati mechi inaendelea.

Kondo amesema, viwanja vingi vimekuwa na usalama mdogo suala linalochangia hata mchezaji kuweza kupata madhara kutoka kwa mashabiki kwani kuna baadhi ya viwanja mashabiki wana uwezo wa kumfanya mchezaji kitu chochote kutokana na ukaribu wa wachezaji na mashabiki hao.

Kondo amesema, TFF inatakiwa kuthamini ligi hiyo kwani inachangia kwa asilimia nyingi kuweza kupata vijana wanaounda timu za ligi kuu na hatimaye timu ya taifa, hivyo kama isipothaminiwa wachezaji wengi watakata tamaa kuweza kushiriki ligi hiyo kutokana na kuwa na miundombinu mibovu ya kimichezo.