Alhamisi , 14th Aug , 2014

Chama cha mpira wa mikono nchini TAHA kimesema kina matumaini makubwa na vikosi vya timu ya wanawake na wanaume ambayo hii leo vimeondoka nchini kuelekea Kampala nchini Uganda kwa ajili ya kushiriki michuano ya Afrika kanda ya Tano

Wachezaji wa mchezo wa mpira wa mikono wakiwa katika moja ya michezo ya Afrika kanda ya tano.

Wachezaji 27, viongozi 4 na waamuzi 2 wa mchezo wa mpira wa mikono Tanzania wameondoka hii leo kuelekea Kampala nchini Uganda ambako watashiriki michuano ya mpira wa mikono kwa nchi za Afrika kanda ya Tano itakayoanza August 16 mwaka huu

Katibu mkuu wa chama cha mpira wa mikono nchini Tanzania Nicolaus Mihayo akizungumza na Muhtasari wa Michezo muda mfupi kabla ya timu hiyo kuondoka hii leo jijini Dar es salaam amesema kwa mazoezi waliyofanya wachezaji hao safari hii wanatarajia timu hiyo itakwenda kufanya maajabu katika michuano hiyo kwani hata morali ya wachezaji iko juu

Aidha Mihayo amesema hategemei kama safari hii kutakuwa na kisingizio cha aina yoyote toka kwa timu hizo kwani zimepata mazoezi ya kutosha na mechi nyingi zakujipima uwezo kwa kucheza na timu mbalimbali za hapa nchini wakati zikiwa kambini kwa maandalizi ya michuano hiyo kitu ambacho kinampa jeuri ya kutamka kuwa safari hii ni mwaka wa Tanzania kuwika katika michuano hiyo.