Ijumaa , 13th Sep , 2019

Robo fainali ya michuano ya Sprite Bball Kings 2019 inaendelea wikiendi hii, ambapo wababe nane watapambana kuwania Shilingi milioni 10.

Sprite Bball Kings 2019

Michezo hiyo itapigwa katika Uwanja wa Ndani wa Taifa, Jumapili ya wiki hii, Septemba 15 ambapo mchezo wa kwanza, Flying Dribblers itacheza na Dream Chasers, K.G Dallas ikicheza na Water Institute, Tamaduni ikicheza na Ukonga Hitmen na mchezo wa Mwisho utashuhudia Mchenga Bball Stars ikipambana na TMT.

Wawakilishi wa Flying Dribblers na Mchenga Bball Stars wamezungumza kuelekea mchezo wao na malengo yao endapo watafanikiwa kushinda ubingwa.

Mwakilishi wa Dream Chasers Jovin Charles, amesema kuwa wamejipanga vya kutosha katika mchezo huo na kwamba wakifanikiwa kushinda milioni 10, watanunua vifaa vya 'Clinic' ya mchezo huo kwa ajili ya kuzunguka nayo mashuleni ili kusaka vipaji.

Kwa upande wa mwakilishi wa Flying Dribblers, Trofimo amesema kuwa kwenye hatua ya robo fainali atahakikisha anafunga pointi nyingi zaidi ya zile alizofunga katika hatua ya 16 bora, ili kuisaidia timu yake kuvuka hatua hiyo na endapo watashinda ubingwa, watatumia pesa hizo katika malengo tofauti.

"Tuna mpango tukishinda hiyo pesa kwanza tunagawana, halafu nyingine tunaweka kwenye mfuko wa timu ili mwaka huu tuweze kuanzisha 'academy' yetu. Tunafikiria zaidi kuwainua wale ambao wanatuangalia ili waweze kufikia kuwa kama sisi", amesema Trofimo.