Jumanne , 17th Jun , 2014

Vijana mkoani Arusha nchini Tanzania wametakaiwa kuacha kupoteza muda mwingi kwenye mijadala ya kutafuta njia za mkato za kurahisisha maisha, badala yake watumie muda na fursa zilizopo kufanya kazi za uzalishaji.

Kamanda wa vijana wa Chama cha Mapinduzi CCM wa mkoa huo Bw. Philemon Mollel amesema hayo alipokuwa akizungumza na vijana hao juu ya tatizo la vijana wengi kuendelea kuendekeza maneno bila vitendo na amewataka kutambua kuwa siasa bila kufanya kazi ya kuwaingizia kipato ndio chanzo cha migogoro na ni adui wa maendeleo.

Naye makamu mwenyekiti wa umoja wa vijana ngazi ya taifa Bi. Mboni Mhita amesema pamoja na umuhimu wa vijana kujitokeza kuwania nafasi mbali mbali za uongozi ukiwemo wa kisisasa, kama hawatajijengea utamaduni wa kufanya kazi hawataweza kutekeleza majukumu yao ipasavyo na kukidhi matarajio ya waliowachagua.