Jumanne , 15th Mar , 2016

Ni nafasi ya kipekee kwa mabondia chipukizi hapa nchini kutoka Mabibo Mkoa wa Dar es Salaam na Ifakara mkoani Morogoro kuonyesha uwezo wao na vipaji vyao katika mapambano yao ambayo yatawawezesha wale watakaofanya vema kwenda kupigana Barani Ulaya.

Bondia Mfaume Mfaume kulia wa mabibo Nakozi gym Dar es Salaam akipambana na Cosmas Cheka wa Morogoro.

Mabondia wa ngumi za kulipwa nchini kutoka Mabibo Nakozi Gym jijini Dar es Salaam wanataraji kuvaana na mabondia wa Ifakara Morogoro katika mapambano maalumu yakusaka rekodi ya kufuzu kucheza mapambano makubwa barani Ulaya.

Wakiongea na hotmix michezo hii leo katika kambi ya mazoezi ya mabondia hao wakiwa na kocha wao Rama Jaa na mratibu wa mapambano hayo Faraji Ngomanya wametamba kushinda na kutwaa nafasi hiyo katika mapambano hayo yatakayofanyika Machi 18 mwaka huu mjini Ifakara Morogoro.

Ngomanya amesema pamoja na mabondia hao kuwania nafasi ya kucheza mapambano makubwa barani Ulaya lakini kubwa ni kuutangaza kwa mara nyingine mchezo wa ngumi za kulipwa katika kitongoji cha Ifakara ambacho zamani kilikuwa kikipata mapambano ya mara kwa mara na baadae kupoteza umaarufu wake na sasa wameamua kwa nguvu zao zote kurejesha mchezo huo mjini humo ili kutoa fursa kwa vijana wa huko kulejea katika medani ya masumbwi.

Kwa upande wake kocha mkuu wa Nakozi Gym ya Mabibo Rama Jaa ambaye anarekodi ya kunoa mabondia wengi na wakafanya vizuri ikiwa ni pamoja na Thomas Mashali amesema mabondia wake wote katika uzito tofauti wamejiindaa vyakutosha ili kuhakikisha wanaibuka kidedea siku huyo na kutwaa nafasi ya kwenda kupambana na mabondia wakubwa wa kimataifa barani Ulaya.

Aidha Jaa amewataka wadau wote wa michezo hasa makampuni kuwekeza na kudhamini michezo hapa nchini hasa mchezo wa masumbwi kwakuwa inanafasi pana yakupeperusha vema bendera ya taifa kimataifa kwani rekodi za hivi karibuni na hata za nyuma zinaonyesha akitolea mfano kina Matumla ambao walikuwa mabingwa wa ngumi kimataifa na dunia na sasa kina cheka nao wanatamba kwa kutwaa ubingwa wa kimataifa.