Jumatatu , 19th Jun , 2023

Baadhi ya wafanyabiashara nchini kupitia sekta binafsi wameitaka serikali kuwa na uharaka katika maboresho ya sheria,kanuni na taratibu ambazo zimekuwa zikisimamia utendaji wa biashara nchini Tanzania ili kuweza kustahimili kwenye soko la ushindani.

Hayo yanajiri katika kongamano la pamoja lililowakutanisha wafanyabiashara kutoka sekta binafsi,wataalam wa maswala ya uchumi kutoka taasisi mbalimbali za kifedha kujadili kwa kina bajeti pendekezwa ya zaidi ya trilioni 44 iliyowasilishwa bungeni na Waziri wa fedha Lameck Mwigulu Nchemba Bungeni Dodoma.

"Leo tumekutana zaidi ya wadau 100 kujadili mwongozo wa bajeti ambayo iliwasilishwa tumeangalia kwenye vipaumbele ambayo serikali imefanya hususani katika sera,mifumo,na kodi hivyo mjadala huu utasaidia wengi" amesema Raphael Maganga Kaimu mkurugenzi TPSF

Baadhi ya washiriki ambao pia ni wafanyabiashara na waagizaji wamesema kwa sasa mazingira ya biashara nchini yameimarika kutokana na serikali kutamani kuona sekta binafsi ikifanya biashara kwa ukubwa.

"Leo tumepata ufafanuzi mzuri rahisi kwa watalaamu wa fedha hii itatusaidia sisi kujua ni maeneo yapi tunaweza kupenya kirahisi zaidi." Amesema mmoja ya wafanyabiashara.

Hata hivyo baadhi yao wachumi na wataalamu wa fedha wamesema lengo ni kuifafanua bejeti hiyo kwa lugha nyepesi ambayo inaweza kumsaidia mfanyabiashara katika kuzifahamu taratibu za kikodi.

Bajeti pendekezwa ya Tanzania ilisomwa bungeni Dodoma na Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba siku ya alhamisi juma lililopita ikiwa na jumla ya shilingi trilioni 44.39