Jumamosi , 23rd Jul , 2016

Mtu mmoja amekutwa akiwa amekufa kifo cha mashaka na kuporwa pikipiki na watu wasiojulikana wilayani Nyamagana, mkoani Mwanza

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, ACP Ahmed Msangi

Taarifa ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza imeeleza kuwa mnamo tarehe 20.07.2016 majira ya saa 02:00 asubuhi katika mtaa wa Maliza kata ya Buhongwa wilaya ya Nyamagana jiji na mkoa wa Mwanza, mtu mmoja aliyejulikana kwa jina la Shabani Haruna Bizeye miaka [32] mwendesha pikipiki (bodaboda) amekutwa akiwa amekufa na kuporwa pikipiki aina ya San LG namba zake bado hazijajulikana na watu wasiofahamika katika mtaa tajwa hapo juu, huku mwili wake ukiwa na majeraha ya kupigwa na kitu kizito pamoja na kufungwa kamba shingoni.

Inadaiwa kuwa marehemu aliondoka nyumbani kwake tarehe 17.07.2016 siku ya Jumapili kwenda kwenye shughuli yake ya kuendesha pikipiki bila kurudi kwake, ndipo ilipofika siku ya Jumatatu ya tarehe 18.07.2016 majira ya 01:30 asubuhi mke wa marehemu bi Hamida Issa alifika kituo cha polisi na kutoa taarifa ya kupotea kwa mumewe,.

Aidha Bi Hamida katika maelezo yake alidai kuwa, pia alipigiwa simu kutoka kwenye simu ya mumewe na mtu asiyemfahamu akitaka apewe kadi ya pikipiki iliyokuwa ikiendeshwa na mumewe.

Kutokana na maelezo ya mke wa marehemu, jeshi la polisi liliweka mtego nyumbani kwa marehemu ndipo alipokuja kijana mmoja aliyejulikana kwa jina la Metusela Robert miaka 17 msukuma torori na mkazi wa Buhongwa akidai ameagizwa aje nyumbani kwa marehemu kuchukua kadi ya pikipiki, ndipo askari walipofanikiwa kumkamata.

Mtuhumiwa aliyekamatwa yupo chini ya ulinzi wa jeshi la polisi huku mahojiano dhidi yake yakiendelea na msako wa kuwasaka watu wengine waliohusika katika mauji hayo bado unaendelea.

Mwili wa marehemu umehifadhiwa hospitali ya rufaa ya Bugando kwa ajili ya uchunguzi