Jumamosi , 25th Apr , 2015

Tume ya uchaguzi nchini Tanzania NEC, imetoa ufafanuzi juu ya suala la upigaji wa kura ya maoni ya Katiba Inayopendekezwa kuchanganywa na uchaguzi mkuu na kusema kuwa mambo hayo hayatafanyika kwa pamoja.

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi NEC, Jaji Mstaafu Damiani Lubuva.

Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Mstaafu Damian Lubuva amesema kuwa mpaka sasa tume haijaamua ni lini kura ya maoni itafanyika ila kwa sasa wanachofanya ni kuendelea na uandikishaji wa Daftari la mpiga kura katika Mikoa iliyobaki.

Jaji Lubuva ameongeza kuwa uchaguzi mkuu wa Rais utakuwepo kama kama ulivyopangwa kuwa ni katika juma la mwisho la mwezi Oktoboa ambapo tayari uandikishaji wa daftari la mpiga kura kwa mfumo wa BVR, utakuwa umekamilika.

Mwenyekiti huyo amesema kuna upotoshaji unaofanywa na baadhi ya vyama vya siasa kwamba tume imesema itachanganya upigaji wa kura ya maoni na uchuguzi mkuu na kusema kuwa suala hilo halina ukweli wowote.

Lubuva amesema kuwa hakuna sheria inayokataza kuchanganywa kwa zoezi hilo kwa wakati mmoja lakini amesema kufanya hivyo kuna changamto nyingi ambazo zitaweza kuharibu chaguzi hizo ikiwa ni pamoja na jinsi ya kufanya kampeni.

Aidha jaji lubuva amekanusha tuhuma za kwamba tume hiyo imeanza uandikishaji katika mikoa ambayo ni ngome ya chama Tawala ili kuhujumu vyama vya upinzani na kusema tuhuma hizo si za kweli na ni upotoshaji na kusema kuwa tume inafanya kazi kwa misingi na taratibu ilizojipangia.

Ameongeza kuwa kwa kuanza mikoa ambayo yamechagua kwa ajili ya zoezi hilo kunatokana na idadi ya watu katika mikoa hiyo kuwa ndogo hivyo na kutokana na vifaa vya kujiandikishia kuwa vichache ndio maana wakaanzia mkoa wa Njombe na sasa wataendelea na mikoa mingine ya Iringa, Lindi, Mtwara na Ruvuma.

Hatua hiyo inafuatia kutokana na shutuma za vyama vya siasa ikiwemo Chama Cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA ambapo naibu Katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Zanzibar Salumu Mwalim, amesema kuwa tume ya taifa Uchaguzi (NEC) isije ikathubutu kuuchezea uchaguzi mkuu kwa kuuchanganya na kura ya maoni ya Katiba Pendekezwa wakithubutu hawata shiriki uchaguzi mkuu Oktoba.

Akizungumza na mamia ya wakazi wa mji wa Njombe Mwalimu amesema kuwa chama hicho hakita shiriki uchaguzi mkuu kama kutatokea uchaguzi mkuu kuchanganywa na kura ya maoni ya Katiba Pendekezwa.

Amesema kuwa kitu hicho kitavunja historia ya nchi na dunia kwani hakijawahi kutokea ulimwenguni pote na kuwa itakuwa ni Tanzania pekee kupiga kura mbili tofauti kwa wakati mmoja.