Alhamisi , 17th Sep , 2020

Kamanda wa Polisi Kanda maalum ya Dar es salaam SACP Lazaro Mambosasa, amesema msaidizi wa Bernard Membe, Jerome Luanda yuko mikononi mwa polisi na ni mzima wa afya hivyo wanaodai ametekwa ni waongo.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, SACP Lazaro Mambosasa.

Amesema hayo leo septemba 17, 2020, akiwa anazungumza na EATV&EA Radio Digital, ambapo amethibitisha kuwa msaidizi huyo yuko mikononi mwa polisi na alikamatwa katika uwanja va Ndege Julius Nyerere.

"Huo ni uongo, uzushi, tumemkamata akiwa Airport pale Julius Nyerere, nasikia wengine wanasema wamemtafuta vituo vyote hawajamuona ni uongo, sisi tupo naye na ni mzima wa afya, tunamshikilia kutokana na kesi zake ambazo hatuwezi kuzitaja", amesema Kamanda Mambosasa.

Hayo yanajiri baada ya Mgombea Urais kupitia chama cha ACT-Wazalendo Bernad Membe, kuandika katika ukurasa wake wa Twitter mnamo Septemba 16 ,20 kuwa msaidizi wake amechukuliwa na watu wasiojulikana, na hivyo akatoa masaa kadhaa ili kupatikana kwa msaidizi wake huyo.