Jumamosi , 21st Jan , 2017

Mamlaka ya chakula na dawa (TFDA) kwa kushirikiana na vyombo vya usalama mkoani Morogoro, imeteketeza shehena ya vipodozi vyenye viambata vya sumu huku vingine vikiwa vimekwisha muda wa matumizi yake

Vipodozi hivyo ni kiasi cha tani 17 zenye thamani ya shilingi milioni 57 mali ya mfanyabiashara Agustino Fikiria Tarimo.

Akizungumza mara baada ya kuteketezwa kwa vipodozi hivyo, Mkaguzi wa kanda ya kati kutoka TFDA Sifa Chamgenzi amewasihi wafanyabiashara kuwa waaminifu na kusema mamlaka ya chakula na dawa haitochoka kuwafuatilia wafanyabiashara wote wanaokiuka  sheria za nchi kwa kuuza bidhaa zilizokataliwa kwakuwa zina viambata  vya sumu ambavyo vina madhara makubwa kwa watumiaji.

Zoezi hilo la kukamata vipodozi hivyo lilichukua siku mbili kutokana na mfanyabiashara huyo kuwa na shehena kubwa nyumbani kwake ambapo alifanya nyumba yake kuwa yadi ya kuwekea bidhaa hizo huku ikiwa ni kinyume na taratibu za uhifadhi wa bidhaa hizo.

Kutokana na hali hiyo baadhi ya wananchi mkoani Morogoro, wamesema kuwa, kuteketezwa kwa vipodozi hivyo ni hatua nzuri, kwani asilimia kubwa ya watumiaji ambao ni wanawake wamekuwa wakiharibika ngozi zao, huku wengine  wakipata magonjwa ya ngozi kwa kuwa vipodozi hivyo wanavyotumia kuwa na vimelea vya sumu.

Msikilize hapa Sifa Chamgenzi - Mkaguzi kanda ya kati TFDA