Jumanne , 24th Mei , 2016

Ikiwa zimesalia siku chache tu kuadhimishwa kwa miaka mitatu ya kifo cha msanii wa Hip Hop na mkali wa Free style Albert Mangwea, Ommy Dimpoz amefunguka mengi kuhusu msanii huyo.

Akiongea kwenye Planet Bongo ya East Africa Radio, Ommy Dimpoz ambaye ni moja kati ya miongoni mwa watu walioathiriwa na msiba wa Ngwair, amemzungumzia msanii huyo na kusema Tanzania imepoteza icon.

“Tanzania ilipoteza icon, mtu ambaye anafanya muziki wa kipekee, mtu ambaye alikuja na flow za kipekee na muziki wa kipekee, pengine muziki ambao watu walikuwa kidogo wanaogopa kuufanya, kwa sababu kulikuwa na aina fulani ya muziki ina trend ya hip hop, lakini akaja na vitu fulani vya kipeke yake”, alisema Ommy Dimpoz.

Pia Ommy Dimpoz amezungumzia suala ambalo anasema lilimuumiza zaidi baada ya kutokea kwa kifo cha Ngwea, na kusema ukweli halisi ni kwamba alikuwa anamkubali sana msanii huyo, tofauti na media zilivyoripoti kwamba alimtukana baada ya kifo chake.

“Kipindi ambacho hata mimi nimepata matatizo yale ya kuandikwa kwamba mimi nimetukana, lakini naweza kusema kwamba mwenyezi Mungu anawafikishaga ujumbe wale waliotangulia au wanasikia, basi mwenyewe kabisa nina uhakika hata aliko anajua kwamba mdogo wangu alikuwa ananipenda”, alisema Ommy Dimpoz.

Albert Mangwea alifariki tarehe 28 Mei 2013 akiwa nchini Afrika Kusini

Albert Mangwea