Alhamisi , 8th Dec , 2016

Wasanii watakaowasha moto katika usiku wa Tuzo za EATV Desemba 10 utakaotikisa anga la Afrika Mashariki kutokea ukumbi wa Mlimani City Jiji Dar es Salaam wameendelea kuwekwa hadhani ambapo leo mkali kutoka Kenya, Wahu, ametangazwa rasmi.

Wahu

Wahu amefanikiwa kuingia katika orodha ya wasanii watakaotumbuiza kwenye usiku wa EATV Awards akiunga na wasanii wengine ambao ni Darassa, Bill Nas, Mourice Krya na Barnaba.

Wasanii wengine wakubwa Afrika Mashariki wanaendelea kutajwa kati ya leo na kesho, endelea kutufuatilia kupitia eatv.tv/awards

Mwanadada huyu mwenye Shahada ya Hisabati kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi ni miongoni mwa wasanii ambao wamefanya vizuri Afrika Mashariki na kufanikiwa kulinda viwango vyao kwa muda mrefu ambapo ameanza kazi ya muziki tangu mwaka 2000 alipotoa ngoma yake ya kwanza iliyokwenda kwa jina la Niangalie.

Wahu, ambaye jina lake kamili ni Rosemary Wahu Kagwi, mke wa msanii mwenzake anayefahamika kwa jina la Nameless waliooana mwaka 2006, na kuendelea kufanya kazi ya muziki kwa kushirikiana ambapo hadi sasa wamefanikiwa kupata watoto wawili wa kike.

Kabla ya kuingia kwenye muziki, Wahu alikuwa ni mwanamitindo, mwandishi wa nyimbo, muigizaji na pia mjasiriamali na katika safari yake ya muziki amewahi kufanya kazi la lebo kubwa ya muziki Kenya ya Ogopa Deejays.

Baadhi ya nyimbo ambazo zimewahi kumuweka vizuri kwenye ramani ya soka ni pamoja na Niangalie, Liar, Sitishiki, Sweet Love, Esha n.k

Mtazame hapa katika ngoma ya NENDA aliyoshirikiana na MOTI-ICE 

 

Tags: