Jumatatu , 30th Nov , 2020

Mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya Senegal na klabu ya Portsmouth ya Uingereza, Papa Bouba Diop amefariki Dunia usiku wa kuamkia hii leo baada ya kuugua kwa muda mrefu akiwa nchini kwao senegal.

Papa Bouba Diop enzi za uhai wake akiichezea Senegal na hii ilikuwa katika fainali za kombe la dunia mwaka 2002.

Rais wa Senegal Macky Sall amesema kifo cha Diop ni pigo kubwa kwa taifa la Senegal, maneno hayo yanakuja baada ya Diop kutoa mchango mkubwa kuisaidia timu yake ya Taifa ya Senegal kuweka rekodi ya kihistoria ya kutinga hatua ya robo fainali ya kombe la Dunia mwaka 2002.

Kwa upande wa nahodha wa Senegal, Sadio Mane amesema ni majonzi kwao kumpoteza mchezaji ambaye alikua kioo kwa vijana wengi akiwemo yeye, huku akisisitiza kwamba ataendelea kuishi katika mioyo yao ingawa ni masikitiko kuwa aliondoka bila ya kuwaaga.

Diop alifunga bao moja dhidi ya Ufaransa ambaye alikuwa bingwa mtetezi dk 30 na kufunga mabao mengine mawili dhidi ya Uruguay kwenye sare ya 3-3 na kuisaidia Senegal kumalizia wapili kwenye kundi A na kutinga robo fainali ambapo waliondolewa na Uturuki.

Nyota huyo ambaye pia amevichezea vilabu vya Fulham, Westham na Birmingham vya Uingereza amefanikiwa kutwaa taji la FA mwaka 2008 akiwa na Portsmouth.

Kocha wake wa zamani, Harry Redknap ametoa pole kwa familia ya michezo.

Kifo cha Papa Bouba Diop kinazidi kuongeza simanzi kwa familia ya michezo baada ya wikiendi hii wanamichezo wakijumuika kumzika aliyekuwa gwiji wa soka nchini Argentina Diego Armando Maradona aliyefariki siku ya jumatano kwasababu ya kupatwa na mshtuko wa moyo.