Jumatatu , 23rd Oct , 2017

Shirikisho la soka nchini TFF limetangaza viingilio vya mchezo wa ligi kuu soka Tanzania VPL, raundi ya nane kati ya wenyeji Yanga SC dhidi ya Simba siku ya Jumamosi kwenye uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam.

Taarifa kutoka shirikisho imebainisha kuwa watazamaji watakaotaka kuketi kwenye jukwaa kuu watapaswa kulipia shilingi elfu ishirini 20000/= ili kuona mchezo huo wa watani wa Jadi.

Watazamaji watakaoketi eneo la mzunguko watalipia shilingi elfu kumi, 10000/= ili kushuhudia mchezo huo unaotarajiwa kuwa na mvuto wa kipekee kutokana na aina ya wachezaji walisajiliwa msimu huu wa 2017/18.

Yanga na Simba zitaingia uwanjani zote zikiwa na alama 15, Simba ikiwa juu kwa tofauti ya mabao hivyo mshindi wa mchezo huo ana nafasi kubwa ya kuongoza ligi huku akisubiri matokeo ya Mtibwa Sugar dhidi ya Singida United.