Jumatano , 19th Jul , 2017

Kocha msaidizi wa timu ya Taifa stars, Fulgence Novatus amesema atahakikisha timu yake inapata ushindi katika mechi yao ya marudiano dhidi ya Amavubi ya Rwanda kwa madai wameyafanyia kazi mapungufu waliyokuwa nayo.

Novatus ameeleza hayo wakati kikosi chake kikiwa kinajiandaa na safari ya kwenda mjini Kigali, Rwanda kwa ajili ya mechi ya marudiano dhidi ya Amavubi katika kuwania tiketi ya kucheza fainali za kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za ndani (CHAN 2018) zitakazofanyikia Kenya.

"Tumeyafanyia kazi mapungufu yaliyojitokeza katika mchezo wetu wa kwanza dhidi ya wapinzani wetu Rwanda katika uwanja wa 'Stade de Kigali', wachezaji wote ni wazima  isipokuwa Shomari kapombe ambaye aliumia  wakati wa mechi ya kwanza. Naamini timu yangu itaibuka na ushindi ili iweze kufuzu kucheza fainali za kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za ndani (CHAN 2018)", amesema Novatus.

Pamoja na hayo, Afisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Alfred Lucas Mapunda amesema kwamba wamekifanyia mabadiliko machache kikosi hicho ili waweze kupata ushindi katika mechi hiyo ya marudiano.

"Tumefanya mabadiliko na sasa Taifa Stars ya kocha Salum Shaaban Mayanga itaondoka Jumatano badala ya Alhamisi, ili kuwaweka sawa kisaikolojia wachezaji pamoja na hali ya utulivu wakiwa nchini Rwanda kabla ya  mchezo huo", amesema Lucas.

Kwa upande wake Nahodha wa Taifa Stars Himid  Mao amewaomba watanzania kwa ujumla waungane na kuiombea timu yao iweze  kutimiza malengo yao ya kufuzu kucheza michuano ya wachezaji wa ligi za ndani(CHAN).