Jumamosi , 21st Dec , 2019

Mtoto mwenye umri wa miaka nane, Ryan Kaji ambaye ni mzaliwa wa Marekani ametajwa na jarida la Forbes kuwa ndiye aliyeingiza pesa nyingi katika mtandao wa YouTube kwa mwaka 2019.

Ryan Kaji

Mtoto huyo ambaye anajishughlisha na kuandaa video za katuni mtandaoni, ametajwa kuwa ameingiza kiasi cha dola 26 milioni ambazo ni sawa na Shilingi bilioni 59 katika kipindi cha mwaka 2019 pekee, ikiwa ni kiasi kikubwa cha pesa kuwahi kupatikana kwa mtu mmoja barani Ulaya.

Katika mtandao wa YouTube, Ryan anamiliki chaneli ijulikanayo kama 'Ryan World', ambayo ina wafuatiliaji takribani milioni 22.9 na kadri chaneli hiyo inayoendelea kukua ndivyo anavyojiingizia kipato kikubwa.

Ryan alianza kazi hiyo akiwa na umri wa miaka mitano na sasa anatengeneza video mbalimbali za kuelimisha. Ametajwa katika tuzo maalum kwa watoto ambao wanakua kwa kasi katika mtandao, maarufu kama 'Kids' Choice Awards for Favorite Social Star'.