Jumapili , 7th Aug , 2022

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe amewaomba radhi wakulima wa zao la parachichi wa wilaya ya Rungwe mkoa wa Mbeya kwa tatizo lililotokea msimu wa kilimo uliopita kuwa halitojirudia tena.

Waziri wa Kilimo Hussein Bashe

Bashe amesema hayo wakati alipopewa fursa na Rais Samia Suluhu Hassan, kusalimia wananchi wa Kiwira wilayani humo katika ziara ya mkuu huyo wa nchi mkoani Mbeya.

Bashe ameeleza msimamo wa Serikali kubadili mifumo ya ununuzi pembejeo za kilimo za ruzuku baada ya Serikali kuja na mpango wa ujenzi wa viwanda vya mbolea nchini.

Amesema msimu uliopita wa kilimo hali ilikuwa mbaya na changamoto kubwa ikiwa ni gharama za pembejeo za kilimo kuwa juu akiwaasa wakulima wa parachichi wilaya ya Rungwe watarajie kuondokana na changamoto hususan ya upatikanaji wa mbegu, pembejeo za kilimo na masoko.