Jumanne , 19th Aug , 2014

Baraza la vyama vya siasia nchini Tanzania limetoa msimamo wake kuhusiana na hatma ya Bunge Maalumu la Katiba ambapo limetaka bunge hilo liendelee.

Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa nchini Tanzania Bw. Peter Kuga Mziray.

Mwenyekiti wa baraza hilo Bw. Peter Kuga Mziray, amesema hayo leo jijini Dar es salaam wakati akizungumzia kuahirishwa kwa kongamano la vyama vya siasa, lililokuwa lifanyike Agosti 23 na 24 mwaka huu kwa ajili ya kujadili mchakato unaoendelea wa kutafuta katiba mpya.

Kwa mujibu wa Mziray, zoezi la kuandika katiba ni mchakato wa maridhiano baina ya pande zote zenye maslahi ndani ya katiba, ambapo amewasihi wajumbe waliosusia vikao vya bunge hilo kurejea bungeni ili kutoa fursa ya kuwepo kwa maridhiano ya kudumu na yenye tija kwa nchi.

Wakati huo huo, Bodi ya mikopo nchini Tanzania HESLB imekiri kuwepo kwa wanafunzi wa elimu ya juu waliocheleweshewa fedha zao za kujikimu kutokana na serikali kutokuwa na fedha.

Naibu Mkurugenzi wa habari na mawasiliano wa bodi hiyo Cosmas Mwaisobwa amesema kuanzia wiki hii malipo yote yatakuwa yamewafikia wahusika na kuainisha kwamba mpaka kufikia July 31 mwaka huu jumla ya maombi mapya ya mkopo 58,037 yamepokelewa.

Mwaisobwa amesema katika kutambua umuhimu wa masomo ya sayansi na kukabiliana na upungufu wa waalimu wa masomo hayo katika ngazi ya shule ya msingi na sekondari, Serikali imetoa fursa ya mikopo kwa wanafunzi 5,000 wanaotarajiwa kujiunga na stashahada hiyo katika chuo kikuu cha Dodoma.