Jumatatu , 12th Jan , 2015

Rais wa Zanzibar Dkt Ali Mohamed Shein ametangaza kufuta gharama zote za shule ya msingi na sekondari kuanzia mwaka ujao wa fedha, ili kuinua sekta hiyo ya elimu kwa upande wa Zanzibar.

Rais Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein amewaongoza Wananchi wa Zanzibar katika maandhimisho ya Miaka 51 ya Mapainduzi ya Zanzibar sherehe ambazo zilifanyika uwanja wa Amani mjini Unguja.

Akihutubia wananchi waliohudhuria katika sherehe hizo, Dkt. Shein amesema takwimu zinaonyesha kiwango cha ukuaji wa uchumi kimeongezeka kutoka 6.4% mwaka 2010 hadi kufikia 7.4 mwaka 2013.

Amesema kuwa Kwa mwaka huu 2015 ukuaji wa uchumi wa Zanzibar unatarajiwa kufikia 7.8%.

Amesema serikali ina mpango wa kuongeza pato la taifa na kukuza ajira, kupitia sekta mbalimbali ikiwemo kilimo kupitia zao la karafuu na shughuli za utalii.

Katika hatua nyingine, Dkt Shein ametangaza kuwa kuanzia mwaka huu, elimu ya Awali na msingi itatolewa bure kwa kuwa serikali itagharamia gharama zote ili kuinua sekta ya Elimu visiwani humo,

Pia kwa elimu ya sekondari, Amesema serikali itagharamia ada ya mitihani ya mwisho, na kwamba taarifa zaidi kuhusu gharama za ada kwa sekondari zitatolewa baadaye.