Jumatatu , 6th Jul , 2015

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt, Jakaya Mrisho Kikwete amewataka viongozi wa dini kuwaelimisha na kuwakemea waumini wao juu ya maadili mabovu yaliyoanza kujitokeza hivi karibuni katika jamii zetu na Nchi kwa ujumla.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt, Jakaya Mrisho Kikwete.

Rais Kikwete ameyasema hayo wakati wa jubilee ya miaka 125 ya Dayosisi ya kaskazini Mashariki yaliyofanyika jijini Tanga ambapo amesema viongozi wa dini wana jukumu zito la kuwaelimisha, kuwakemea na kuwarudisha kwenye maadili mema wanakondoo wao waliopewa kuwachunga.

Aidha ameongeza kuwa kwa upande wa serikali huwa iko tayari kutekeleza ipasavyo wajibu wa kisheria katika makosa mbalimbali ambayo wananchi wanaweza kuyafanya tofauti na upande wa madhehebu ya dini hutumia lugha ya kuwaelimisha kwa kuwataka waumini watii amri za Mungu.

Sambamba na hayo pia amewaomba viongozi wa dini kuiombea nchi katika mwaka huu wa uchaguzi pamoja na kuwakemea wagombea watakaotumia pesa ili kununua ushindi wa madaraka na kufanya ubaguzi wa rangi, kabila na dini ili kuwajenga kisiasa.

Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Dayosisi ya Kaskazini Mashariki Steven Munga amesema kuwa eneo hilo lilitumika kipindi hicho tangu wamisionari walipofika kwa mara ya kwanza kwaajili ya kueneza dini na kukomboa maisha ya watu waliokuwa watumwa ambao walichukuliwa na kutunzwa.