Jumatatu , 8th Sep , 2014

Mbunge wa Jimbo la Nzega mkoani Tabora nchini Tanzania Dkt. Khamis Kigwangala,jana ametangaza rasmi kuwa atawania nafasi ya urais katika uchaguzi mkuu ujao kupitia chama chake cha CCM.

Mbunge wa Jimbo la Nzega mkoani Tabora nchini Tanzania Dkt. Khamis Kigwangala.

Dkt. Kigwangala ametangaza uamuzi huo jijini Dar es Salaam ikiwa ni wiki moja tangu waziri mkuu Mizengo Pinda naye atangaze hatua kama hiyo, ambapo kwa mujibu wa Kigwangala, urais kwake yeye ni kuwatumikia Watanzania na kwamba anataka awe rais wa kwanza kuongoza Tanzania ikiwa taifa tajiri.

Kwa mujibu wa Dkt Kigwangala, masuala matatu yatakuwa ya kipaumbele kwake iwapo atateuliwa ndani ya chama chake na baadaye kuchaguliwa na Watanzania kuwa rais ni huduma za kijamii, miundombinu, haki na usawa pamoja na suala la utawala bora kwa watendaji na watumishi wa umma.

Katika hotuba yake ndefu kwa waandishi wa habari, Dkt Kigwangala amesema anataka kugombea urais kwa sababu anajua mahitaji na shida wanazokumbana nazo Watanzania na kwamba hajaamua kugombea nafasi hiyo kutokana na shinikizo la mtu yoyote wala makundi yanayotajwa kuwa ni kambi za baadhi ya wanaowania nafasi hiyo.