Jumatano , 4th Dec , 2019

Mahakama ya Wilaya ya Pangani mkoani Tanga, imemuhukumu Kijana Mahadi Elias maarufu kwa jina Maiko, mwenye umri wa miaka 22 mkazi wa Kijiji cha Stahabu wilayani humo, kifungo cha miaka 30 jela kwa tuhuma za kumbaka mwanamke mwenye umri wa miaka 27.

Hukumu hiyo imetolewa Jana Disemba 2, 2019, na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo Joel Mnguto, ambapo Maiko amehukumiwa kwenda jela miaka 30 na kutakiwa kumlipa fidia mwanamke huyo ya Shilingi laki tatu kwa kosa la kufanya kitendo cha ubakaji huku akijua kufanya hivyo ni kosa kisheria.

Inadaiwa Maiko alitenda kosa hilo April 5, 2019, majira ya usiku, katika kijiji cha Sange, baada ya kumvamia mwanamke huyo chumbani alikokuwa amelala na kisha kumuingilia kimwili bila ridhaa yake, huku akimuwekea kisu shingoni na kumtisha kuwa asipokubali atamuuwa kwa kumchinja.

Awali mtuhumiwa alikana kosa hilo ambapo upande wa mashtaka ulilazimika kuleta mashahidi 11 ili kuthibitisha kosa hilo, ambapo pamoja na mshtakiwa kujitetea, ushahidi ulipokamilika mtuhumiwa alikutwa na hatia.