Jumanne , 9th Jul , 2019

Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli, amempongeza faru Rajabu, ambaye ni mtoto wa Faru John, kwa juhudi zake za uzalishaji na kuzidi kuongeza idadi ya faru hadi kufikia faru140, katika hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Rais Magufuli ameyabainisha hayo leo Julai 9, wakati wa Uzinduzi wa Hifadhi ya Taifa ya Burigi, iliyopatikana mara baada ya mapori matatu ya akiba kuunganishwa, likiwemo pori la Burigi, Biharamulo na Kimisi Wilayani Chato Mkoani Geita.

''Hakuna budi kupongeza kazi kubwa na nzuri iliyofanywa na faru rajabu, mtoto wa faru John naambiwa kwasasa amezalisha watoto 40, nadhani wajina wangu john alikuwa hajitumi vizuri''.

Rais Magufuli amemuagiza waziri wa Maliasili, kuhakikisha anawachukulia hatua stahiki viongozi wa Maliasili, ikiwemo kuwafukuza kazi, endapo itatokea upotevu wa wanyama katika hifadhi mbalimbali za wanyama.

Aidha wakati wa Uzinduzi huo, Rais Magufuli amekabidhiwa tuzo mbili, ikiwemo ya hifadhi ya Taifa ya Serengeti pamoja na ya Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro, pamoja na zawadi ya Taswira ya Baba wa Taifa Hayati Mwalim Julius Nyerere, kama zawadi ya kumthamini na kuutambua mchango wake wa Uhifadhi wa Mazingira.