Alhamisi , 21st Jan , 2016

Rais waTanzania Dkt. John Magufuli amewasimamisha kazi Makamisha wa Uhamiaji ili kupisha uchunguzi, kufuatia dosari alizozibaini Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mheshimiwa Charles Kitwanga alipotembelea Idara ya Uhamiaji hivi karibuni.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt. John Pombe Magufuli.

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amezitaja dosari hizo kuwa ni pamoja na tuhuma za rushwa, ukusanyaji mbaya wa maduhuli ya serikali, ukiukwaji wa taratibu za manunuzi na utendaji mbovu huku akiwataja Makamishana hao ni Kamishna Mkuu wa Uhamiaji Bw, Sylvester Ambokile na Kamishna wa Uhamiaji anayeshughulikia Utawala na fedha Bw, Piniel Mgonja

Balozi Sefue amesema watendaji hao wakuu wa Uhamiaji wamesimamishwa kazi mara moja hadi hapo uchunguzi utakapokamilika na kwamba endapo watabainika kutokuwa na makosa Rais ataamua hatma yao.

Katika Hatuanyingine Rais John Pombe Magufuli amemrejesha Bw, Eliakim Chacha Maswi kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara, baada ya kukamilisha kazi maalum aliyomtuma kuifanya katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Kabla ya kurejeshwa kuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara Bwana Maswi aliteuliwa kuwa Kaimu Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amesema, Rais Magufuli amefanya mabadiliko hayo kwa lengo la kumtafuta mtu mwenye utaalamu wa kuendeleza kazi iliyofanywa na Bwana Maswi.