Jumanne , 1st Sep , 2015

Aliyekuwa mgombea urais kupitia CCM, Januari Makamba amesema kuwa vyama vya upinzani havipaswi kupewa uongozi wa nchi kwa kuwa havina sera zinazoeleweka wala demokrasia ya kweli.

Aliyekuwa mgombea urais kupitia CCM,na mbunge aliemaliza muda wake wa jimbo la Bumbuli Mh. Januari Makamba

Makamba ametoa kauli hiyo mjini Dodoma wakati akizindua kampeni za mgombea ubunge wa jimbo la Dodoma Mjini, Anthony Mavunde katika viwanja vya Barafu vilivyoko mjini humo na kusema kuwa kinachofanyika kwenye vyama vya upinzani ni maigizo na siyo mabadiliko ya kweli kama wanavyojinadi.

Amesema kuwa kwa muda mrefu upinzani nchini umejijengea jina kwa kauli zao za kupinga vitendo vya ufisadi na rushwa lakini badala yake wamewachukua watu waliokuwa wanawaaminisha Watanzania kwa muda mrefu kuwa ni mafisadi na kuwa wagombea wao wa nafasi nyeti ya Urais.

Aidha amesema kuwa hata njia alizotumia mgombea Urais kupitia CHADEMA, Edward Lowassa kujiunga na chama hicho kilijawa na mizengwe mingi kutokana na uroho wa madaraka alionao.

Amesema mgombea Urais kupitia CCM, John Magufuli ndiye mtu pekee wa kuaminiwa na kupewa nchi kutokana na uchapakazi wake na hana kashfa yoyote ya ufisadi wala rushwa.