Jumatano , 30th Sep , 2015

Watu 62 akiwemo Mgombea Ubunge jimbo la Iringa mjini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA, Mchng. Peter Msigwa wanashikiliwa na jeshi la Polisi mkoani humo kwa tuhuma za kuufanyia fujo msafara wa Mgombea Urais wa CCM, Dkt. John Magufuli.

Mgombea Ubunge Jimbo la Iringa Mjini Mchungaji Peter Msigwa akisindikizwa Mahakamani, (Picha hii ni tukio lililotokea siku za nyuma halihusiani jinsi alivyokamatwa siku ya Jana)

Habari zilizothibitishwa na Jeshi la Polisi Mkoani humo zinasema kuwa wanamshikilia mbunge huyo kuhusika kwa namna moja ama nyingine katika kushawishi watu hao kufanya fujo.

Aidha mtoa taarifa huyo wa jeshi la polisi ameongeza kuwa kwa uchunguzi wa awali zinaonesha kuwa mchungaji huyo aliaandaa njama za kuwashawishi vijana hao kuwashambulia wanachama wa CCM, wakati mgombea wao urais alipofanya mikutano yake ya kampeni mkoani humo.

Wakati huohuo mgombea urais huyo aliendelea na ziara yake katika jimbo la Isimani, Mtera kuelekea Dodoma huku akiwataka watanzania kumpa kura na kumuamini kwa kuwa ataunda serikali yenye uadifu na kufanya kazi.

Aidha Mh. Magufuli amesema kuwa endapoa atapewa ridhaa hiyo pia serikali yake itawajali wanachuo wanaomaliza elimu ya juu kwa kuwapa mikopo ambayo itakayowawezesha kuanzisha makampuni ili kuongeza wigo wa soko la ajira.