Jumatatu , 26th Feb , 2018

Sio mara ya kwanza kusikia madaktari wasio na mipaka, au meli zinazofanya ziara zake sehemu mbalimbali duniani kutoa huduma za matibabu kwa watu wasiojiweza na hata wale wenye uwezo.

Mercy Ship Africa  ni moja ya meli kubwa duniani, ambayo inafanya ziara zake nchini Afrika na kutoa huduma mbali mbali za kiafya kwa watu wasio na uwezo wa kupata huduma bora za afaya na matibabu yake.

Ilianzishwa mwaka 1978 na Don Stephen akiwa na mkewe Deyon Stephens  lakini ile inayotoa huduma Afrika ilianzishwa mwaka 1999 kwa misaada ya watu mbali mbali, na kutengenezwa maalum kwa ajili ya hospitali inayotembea ili  kutoa msaada wa matibabu kwa nchi mbali mbali barani Afrika.

Mercy Ship haipo ya Afrika pekee, zipo 4 duniani ikiwemo ya kwenda visiwa vya Caribean, ya kwanza kabisa kuanzishwa inayoitwa 'Anastasis' na Good Samaritan ambayo pia ilikuwa ikizunguka duniani.

Kwenye meli hii kuna timu ya madaktari bingwa zaidi ya  450 waliotoka nchi tofauti tofauti duniani, ambao wamekuwa wakifanya miujiza kwa kubadilisha maisha ya watu ambao pengine walikuwa wameshakata tamaa, na kuwapa tumaini jipya na kujiona ni miongoni mwa jamii inayoishi.

Mpaka sasa meli hiyo imeshafanyia upasuaji zaidi ya watu 84,000 Barani Afrika kwenye nchi tofauti tofauti ikiwemo Benin, Togo, Camerron na nyinginezo, na bado inaendelea kutoa huduma hizo, ikiwemo kunyoosha miguu ya watu mbali mbali ambao waliamini kuwa ni walemavu kwa maisha yao, na kuokoa maisha ya watoto ambao hali zao walikuwa kwenye hatari ya kufa bila gharama yoyote ya matibabu.
 

Binti ambaye amefanyiwa upasuaji wa kunyoosha miguu
Kijana mabye amefanyiwa upasuaji wa kunyooshwa miguu
Mwanamke ambaye amefanyiwa upasuaji wa uvimbe wa shingo
Mtoto aliyejulikana kwa jina la David, ambaye naye amefanyiwa upasuji wa miguu.