Jumanne , 21st Apr , 2015

Mkuu wa Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera, Luteni Kanali Mstaafu Benedict Kulikila amefariki dunia jana katika hospitali ya taifa ya Muhimbili alikokuwa amelazwa.

Kifo cha Luteni Kanali Kulikila zimethibitishwa na Mkurugenzi wa Idara ya Habari -Maelezo, Assah Mwambene, ambaye amesema marehemu amefariki kwa ugonjwa wa shinikizo la damu.

Mwambene amesema mwili wa marehemu umeagwa leo katika hospitali kuu ya jeshi Lugalo jijini Dar es Salaam na kwamba maziko yake yatafanyika April 23, nyumbani kwake Kola Hill mkoani Morogoro.

Msemaji wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania – JWTZ, Meja Joseph Masanja, amesema shughuli ya kuagwa kwa mwili wa marehemu Kulikila zimeongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiongozana na Waziri Mkuu Mizengo Pinda.

Aidha, Masanja amesema viongozi wengine waandamizi wa serikali na jeshi wamehudhuria hafla ya kuuaga mwili wa marehemu Kulikila ni Mnadhimu mkuu wa jeshi la wananchi Samweli Ndomba.