Jumatatu , 25th Jul , 2016

Watendaji katika sekta ya Afya katika Halmashauri ya wilaya ya Iringa wameiomba Bohari ya Dawa nchini (MSD), kushirikiana na watendaji hao katika kutafuta namna bora ya kusambaza dawa na kupunguza malalamiko ya upungufu wa dawa kwenye vituo vya Afya

Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Lauren Bwanakunu

Wakizungumza katika kikao cha kujadili njia bora za upatikanaji wa dawa pamoja na vitendanishi vituoni wamesema wakati sasa umefika kwa uongozi wa bohari hiyo kusikiliza ushauri wa wadau hao na kupendekeza namna bora zaidi ya kutatua changamoto zilizopo.

Kikao hicho kimeitishwa na Shirika la Maendeleo ya Jamii TACOSODE, linalotekeleza mradi wa kushirikisha wananchi kwenye Sekta ya Afya kwa lengo la kubaini vikwazo vya sekta hiyo na kutafuta ufumbuzi wa pamoja.

Akizungumzia hoja hizo Afisa huduma kwa wateja kutoka MSD, Mkoani Iringa Henri Luanda, amekiri kuwepo kwa changamoto nyingi katika usambazaji wa dawa ingawa amesema chanzo ni ubovu wa utoaji taarifa za mahitaji halisi ya dawa vituoni huku Mtendaji wa TACOSODE, akitaka serikali kuboresha zaidi sekta hiyo.