Jumanne , 7th Jul , 2020

Mtia nia wa kugombea nafasi ya Urais kupitia CHADEMA Dkt Mayrose Majinge, ameahidi kuwa endapo chama chake kitampa ridhaa ya kugombea nafasi hiyo, basi atahakikisha kila Mtanzania anayetaka utajiri anaupata kwani ataboresha fursa za ujasiriamali.

Mtia nia wa kugombea nafasi ya Urais kupitia CHADEMA, Dkt Mayrose Majinge.

Kauli hiyo ameitoa hii leo Julai 7, 2020, wakati akichukua fomu ya kuomba uteuzi wa chama hicho ili aweze kupewa ridhaa ya kupeperusha bendera ya Urais katika Uchaguzi Mkuu ujao mwezi Oktoba.

"Kama chama changu kitanipitisha ninaahidi kila Mtanzania kuwa na uhakika wa chakula na matibabu, ahadi yangu ya pili ni kuwezesha kila Mtanzania kupata elimu yenye kujenga maarifa na uwezo mkubwa wa kufikiri ili kutumia fursa zilizopo kwa uhuru na furaha, ahadi nyingine ni kuwezesha kila Mtanzania mwenye kutaka utajiri anaupata kwa kuboresha fursa za ujasiriamali na mitaji ya kutosha katika sekta binafsi na kutengeneza mazingira rafiki kwa wafanyabiashara wote" amesema Dkt Mayrose.

Dkt Mayrose Majinge ndiye mwanamke wa pekee kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), aliyejitokeza kutangaza nia ya kuwania nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.